Wapewa elimu matumizi nishati ya kupikia

TAASISI ya Wanawake Wafanyabishara Tanzania (TABWA), imetoa elimu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa wajasiriamali zaidi 100 lengo likiwa ni kuunga mkono mpango wa miaka 10 wa serikali wa kuachana na matumizi ya mkaa na kuni.
Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi hiyo, Noreen Mawala, wakati wa kongamano la utoaji wa elimu kwa wajasiriamali, liliofanyika jijini Dar es Salaam.
Amesema taasisi hiyo imefanikiwa kutoa elimu kwa wajasiriamali hao ambao ni mama lishe na wakaanga chips kutoka katika mikoa ya Morogoro, Pwani, Dar es Salam na Songwe.
Amesema lengo kubwa la taasisi hiyo ni kuhakikisha inauunga mkoni mpango wa miaka 10 wa serikali wa kuondokana na matumizi ya nishati za kuni na mkaa, ambazo kwa kiasi kikubwa zimeendelea kuathiri mazingira na kwamba huwafikia wajasiriamali 6000 katika mikoa 15 nchini.
“Leo tumetoa elimu kwa mama lishe na wakaangaji wa chips zaidi ya 100 juu ya athari za matumizi ya nishati za kuni na mkaa..mpango wa serikali kwa sasa baada ya miaka 10 ni kuhama katika matumizi ya mkaa na kuni, hivyo elimu kama hii ni muhimu,”amesema.
Amesema licha ya kuendelea kutoa elimu changamoto ni uelewa ni mdogo kwa jamii kuhusina na matumizi ya nishati safi za kupikia na kwamba bado elimu inahitajika zaidi husuani kwa maeneo ya vijijini.
Awali akizungumza katika kongamano hilo, mtaalamu wa masuala ya nishati, kutoka Wizara ya Nishati, Anitha Ringia, alisema kutokana na matumizi ya nishati ya kuni na mkaa yamekuwa yakichangia ongezeko la magonjwa sugu na kusababisha vifo.
“Ripoti zinaonesha watu zaidi ya 33,000 hufariki kwa mwaka kutokana na magonjwa sugu ikiwemo homa,kikohozi, homa za mapafu na mengine mengi na pamoja na kuwepo kwa sababu nyingine, ila matumizi ya kuni na mkaa yanachangia vifo,”alisema.
Nao baadhi ya wajasiriamali walionufaika na mafunzo hayo, walisema elimu hiyo itawasaidia kutumia nishati mbadala na kuiomba serikali kupunguza gharama za gesi.
“Changamoto gesi gharama yake ni kubwa ikilinganisha na mkaa na kuni licha ya kwamba tumefundiahwa kwamba zinaleta athari kiafya, lakini gharama za gesi ni kubwa tunaomba serikali kupunguza,”alisema Eva Mwakalinga.