DAR ES SALAAM; Msanii wa Bongo fleva nchini Oscar Lello ‘Whozu’, leo ameitikia wito aliokuwa ameitwa na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata), baada ya kuposti kipande cha video kinachodaiwa hakina maadili.
Akizungumza na waandishi wa habari, baada ya kuitikia wito huo, Whozu amesema:”Niiitwa nimeitikia wito kwa walezi wetu katika tasnia ya sana,a nimeongea nao, nilikosea kuna mtu alituma video isiyo na maadili kwenye akaunti yangu kwa bahati mbaya.
“Kama walezi wamenieleza nimewaelewa, video nilishafuta lakini ilikuwa tayari imeshasambaa, hivyo naomba radhi sitarudia tena ilikuwa bahati mbaya.”
Basata hivi karibuni lilisema kumekuwa na wimbi la wasanii kuwa na tabia ya kupiga picha na kujirekodi au kurekodiwa video zenye maudhui ambayo ni kinyume na maadili ya Kitanzania.
“Baraza linatoa onyo kali kwa wasanii wote kuacha tabia ya kujirekodi au kurekodiwa na kusambaza picha au video zisizo na maadili kwenye mitandao ya kijamii, kwani kufanya hivyo ni kinyume cha sheria na kanuni za uendeshaji wa shughuli za sanaa na maadili ya Kitanzania.
“Baraza halitasita kuchukua hatua kali ikiwemo kufutiwa leseni na kibali cha kujishughulisha na kazi ya sanaa kwa wote watakaoenda kinyume na tamko hili, kwani itatafsiriwa kuwa ni uvunjaji wa sheria,” amesema.