MTWARA; MAMLAKA ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA), imeanza kutekeleza agizo la Rais Samia Suluhu Hassan la kusafirisha korosho zinazozalishwa mikoa ya kusini kupitia Bandari ya Mtwara.
Agizo hilo limeanza kutekelezwa, ambapo TPA kupitia meli ya Makasha ya CMA-CGM Saigon imeleta makasha matupu 225 kwa ajili ya kusafirisha korosho kupitia Bandari ya Mtwara.
Meli hiyo imetia nanga katika gati jipya leo, ambapo ilishuhudiwa na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na baadhi ya wafanyabiashara wa zao la korosho kusini.
Meneja wa Bandari ya Mtwara Ferdinand Nyath amesema mamlaka ya bandari imejipanga kuhakikisha kwamba agizo la Rais linatelezeka kwa ufanisi.
“Bandari ya Mtwara ilishajipanga na tumejiandaa kuhakikisha kwamba tunahudumia shehena ya korosho kwenda nje,” amesema.
Kwa upande wa vifaa, Nyath amesema serikali imenunua mitambo ya kuhudumia shehena hizo na kwamba bandari ipo tayari kupokea meli kwa ajili ya kuhudumia shehana za Korosho.
Amesema kampuni nyingi zimejitokeza kuleta makasha matupu kwenye bandari ya Mtwara kusafirisha korosho.
Kwa mujibu wa Nyath, mpaka kufikia mwezi Novemba kutakuwa na meli saba ambazo zitaleta makasha 400 Kwa kila meli.
Comments are closed.