Mkuu wa mikoa Kilimanjaro tayari ametiki

MIKOANI: WAKUU wa mikoa mbalimbali wamejitokeza kushiriki upigaji kura katika mikoa yao kwa kuchagua viongozi wanaowataka katika uchaguzi wa Rais, wabunge na madiwani.
Mkuu wa Mkoa Wa Kagera, Hajath Fatma Mwassa ameshiriki upigaji kura katika kituo cha Airport ya zamani kilichoko mjini Bukoba.

Mara baada ya kupiga kura ameviambia vyombo vya habari kuwa ameridhishwa na maandalizi ya uchaguzi katika sehemu za vituo.
Pia Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela ameshiriki upigaji kura akiwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita, Mohamed Gombati katika kituo cha kupiga kura cha Shule ya Sekondari ya Geita (GESECO) iliyopo mjini Geita.

Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu, ametimiza haki yake ya kikatiba kwa kupiga kura huku akiwataka wanaanchi wajitokeze kwa wingi kushiriki katika zoezi hilo.
Babu amepiga kura leo asubuhi katika kituo cha kata ya Kilimanjaro Manispaa ya Moshi ambacho ni kimoja kati ya vituo 3074 vilivyopo mkoani hapa.
Mkoani Mtwara, Mkuu wa Mkoa, Patrick Sawala ametekeleza haki ya kikatiba ya kupiga kura katika kituo kilichopo Chuo cha Utumishi wa Umma Shangani Manispaa ya Mtwara Mikindani mkoani humo.

Mkuu huyo wa mkoa ameungana na wananchi wengine waliojitokeza asubuhi mapema kwenye vituo mbalimbali vya kupigia kura kwa ajili ya kushiriki zoezi hilo linalofanyika nchini.
Akizungumza baada ya kupiga kura, Sawala amepongeza maandalizi yaliyofanywa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) na kuwataka wananchi kuendelea kujitokeza ili kutimiza haki yao ya kikatiba.



