Wamiliki hoteli wapewa neno AFCON 2027

ARUSHA: Wamiliki wa hoteli nchini wametakiwa kujipanga na kuboresha huduma zao ikiwemo miundombinu ya malazi,kuelekea AFCON 2027 ambapo inakadiriwa Tanzania itapokea watalii laki tatu kwa siku.
Akizungumza Aprili 23 wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya miundombinu ya malazi katika Hifadhi ya Pori Tengefu Mto wa Mbu, wilayani Monduli, mkoani Arusha, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Ashatu Kijaji amesema Tanzania inatarajiwa kupokea idadi kubwa ya watalii kutoka ndani na nje ya nchi.

Dk.Kijaji amesema kuwa mashindano ya AFCON 2027 yatatoa fursa kubwa ya kiuchumi kwa nchi, hivyo ni wajibu wa wadau wa sekta ya utalii, hususan wamiliki wa hoteli na loji kuhakikisha wanatoa huduma bora zinazokidhi viwango vya kimataifa.
“Ni muhimu kwa kila mmiliki wa hoteli kuhakikisha anajiandaa vyema ili kuwahudumia wageni kwa ubora unaostahili,” amesema Dk. Kijaji.
Aidha, amesema kuwa ujio wa AFCON 2027 katika ukanda wa Afrika Mashariki, ikiwemo Tanzania, ni fursa adhimu kwa wananchi kunufaika kiuchumi na kukuza sekta ya utalii.

Kwa upande mwingine, amesema uongozi wa Hifadhi ya Pori Tengefu Mto wa Mbu unapaswa kuboresha miundombinu na huduma zake ili kuongeza mvuto kwa watalii na kuwapatia uzoefu bora wanapotembelea hifadhi hiyo.
Katika ziara hiyo, Dk. Kijaji alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ubora wa huduma ili kuendana na mahitaji ya soko la kimataifa.

Mashindano ya AFCON 2027 yanatarajiwa kufanyika katika nchi za Afrika Mashariki, ambapo Tanzania ni miongoni mwa wenyeji wa tukio hilo kubwa la michezo barani Afrika, linalotarajiwa kuvutia maelfu ya wageni kutoka sehemu mbalimbali duniani.



