Samia: Vijana lindeni amani

MGOMBEA urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Samia Suluhu Hassan ameagiza vijana walinde amani na waipende nchi yao.
Samia alisema hayo katika Kata ya Runzewe, Wilaya ya Bukombe mkoani Geita wakati wa mkutano wa kampeni jana.
“Ninalotaka kuwaambia vijana nchi inayoitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ipo moja peke yake, tangu nchi hii imeundwa tumepigana vita moja tu na Idi Amin na kwa sababu alituchokoza,” alisema.
Samia alitoa wito kwa vijana wawe wazalendo, waipende nchi yao na wasije kurubuniwa kwa namna yoyote wakaharibu nchi yao.
Alisema miaka yote nchi ipo salama na kuahidi uongozi wake utaendelea kulinda amani waliyoikuta.
“Tangu tukiwa wadogo tulizaliwa, tukakuzwa kwenye amani, tumekuwa wakubwa tunaendesha nchi hii bado tunalinda amani… Vijana twendeni tukalinde amani yetu, tusikubali kwa hali yeyote kushawishiwa kuharibu amani yetu, hamtakwenda kwenye kuchimba (madini) hamtakwenda kwenye muziki, hamtafanya chochote amani ikiharibika,” alisema Samia.
Alisema Tanzania ni nchi inayoheshimiwa kutokana na sifa ya amani na maendeleo.
“Wakati nakuja huku (Geita) nilisimama Kahama ambako kuna mchanganyiko wa watu kutoka nchi jirani wote wapo pale wamefuata biashara, wamefuata maisha, wamefuata amani, mkiharibu ninyi kwenu kama wale wanakuja huku nyie mtakwenda wapi, hamtapata pa kukimbilia, niwaombe kwa njia yeyote ile asije mtu akasema fanyeni hiki, fanyeni hiki mkavuruga amani ya nchi yetu na mkaharibu sifa nzuri ya nchi yetu,” alisema Samia.

Alisema serikali imewapa zawadi ya uwanja wa michezo wa kisasa ili wanapomaliza shughuli za kiuchumi wawe na sehemu ya kuburudika.
“Tunajenga kiwanja kikubwa cha kisasa cha michezo Ushirombo, kiwanja kizuri sana cha michezo ambacho Bukombe itaingia kwenye ramani ya wilaya ambazo kama mechi za Ligi Kuu ya Tanzania Bukombe kutakuwa na kiwanja,” alisema Samia.
Aliongeza: “Hiyo ni zawadi ya serikali yenu kwa vijana, tunawapa kazi za kiuchumi lakini tunawapa maeneo ya kufanyia michezo na kuburudika… Serikali tunawapenda sana na tunawaomba na nyinyi muipende nchi yenu”.



