Wenje: Siwezi kuzama huku ninaona

KAGERA: KADA mpya wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ezikia Wenje amesema hajutii uamuzi wake wa kujiunga na chama hicho kwani amejionea kwa vitendo mambo makubwa yaliyofanywa na chama hicho kwa siku nne alizokaa CCM.
Akizungumza leo Oktoba 16, Mjini Bukoba mkoani Kagera wakati wa mkutano wa mgombea urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi ( CCM) Dk Samia Suluhu Hassan, Wenje amesema anafahamu kuna watu wanamshangaa kujiunga na CCM lakini yeye amefuata maendeleo.
” Ninaomba niwaaambie kitu wakati nikiwa kwenye chama changu cha zamani ( CHADEMA) tulikuwa tukikaa vikao vya mara kwa mara, sasa ilikuwa inakuja karatasi tunaita paper ya siasa ilikuwa ikionesha hali ya siasa nchini ikibainisha mambo yanayofanywa na Serikali, tuliona miradi mingi ilifanywa lakini sisi tulikuja na hoja ya kutaka maendeleo ya mtu mmoja mmoja, sasa cha kushangaza kila sehemu niliyopita ninaona maendeleo yaliyofanywa nimebaki ninashangaa” amesema Wenje.
Aidha Wenje ameeeleza kuwa anafahamu kuna watu bado wanahoji uamuzi wake wa kujiunga na CCM lakini anaamini kila mmoja ataelewa kuwa alifanya maamuzi sahihi.
“Kuna watu wanashangaa kwanini nipo CCM, niwaambie tu ukweli, mimi siwezi kuzama huku ninaona, lengo la vyama vya siasa ni kwenda kushika dola na tunafahamu kuwa kuna uchaguzi ambao kila mahali uchaguzi ni mchakato na ni lazima ufuate ule mchakato ili uweze kushiriki lakini chama changu cha zamani kilikiuka hakikufuata hiyo michakato tunaishia kulaumu Serikali” amesema Wenje.
Amehimtimisha kwa kusema kuwa anauona mwanga katika sekta mbalimbali hivyo amewaomba wananchi kumchagua Dk Samia Suluhu Hassan katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 29 ili andeleze kazi aliyokwisha ianza.



