Umuhimu wa lishe bora katika kutibu utapiamlo

MAENDELEO ya Taifa lolote pamoja na mambo mengine yanahitaji uwepo wa watu (nguvu kazi) wenye afya njema na uwepo wa lishe bora ili kuwawezesha kufanya kazi kwa bidii na tija.
Kwa kutambua hilo serikali imeendelea kutekeleza Mpango Jumuishi wa Pili wa Taifa wa Lishe kwa mwaka 2021/2022-2025/2026 katika sekta mtambuka kuhakikisha wazazi wanatekeleza na watoto wanafikiwa na lishe bora.
Mmoja wa wazazi wa kata ya Kisuke, Halmashauri ya Ushetu, Zanuda Shija anasema amekuwa akipata elimu ya lishe kwenye kituo cha Afya anapopeleka watoto wake kliniki na wakati mwingine wahudumu wa afya ngazi ya jamii wamekuwa wakitoa elimu hiyo pia.
Anabainisha hayo wakati wa mahojiano yake na HabariLEO hivi karibu. Naye Daudi Jenga anasema wazazi wengine wamekuwa wakidharau elimu ya lishe wanayopatiwa bila kujua kwamba lishe sahihi ni jambo muhimu kwa afya ya watoto.
Anasema kwa sasa amejua kuwa mtoto akipatiwa matunda na ugali au uji kwa unga usiokobolewa inatosha kumwepusha kupata magonjwa na kumpa shibe ya muda mrefu. Mhudumu wa Afya ngazi ya jamii Vicent Mahona anasema wamekuwa wakitoa elimu ya lishe kuhakikisha wajawazito na watoto wanafuata kanuni bora kuanza upishi hadi ulaji na madhara yanayotokea kwa mjamzito na mtoto wasipopata lishe bora.
“Tunawaeleza vyakula vipatikane kwenye maeneo yao wasilazimishe vile ambavyo havipatikani kwa urahisi ili kila kaya iweze kumudu chakula hicho na kuepusha madhara ya magonjwa na baadaye kutumia gharama kubwa kwenye matibabu,” anasema Mahona.

Ofisa lishe wa Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu, Mohamed Mkoko akiongea kwenye kikao cha robo ya pili cha lishe anasema watoto 11 wenye ugonjwa wa utapiamlo walitoroshwa na wazazi wao wakati wakiendelea na matibabu.
Anaongeza kuwa wamefanya jitihada za kuwatafuta bila mafanikio na wala hakuna taarifa za mahali walipo. “Mpaka sasa hatufahamu kama bado wazima au wameshakufa, sababu kubwa imebainika wazazi hao kushindwa kujihudumia wakati watoto wakipatiwa matibabu,” anasema Mkoko. Mkoko anasema matibabu ya mtoto mmoja mwenye utapiamlo serikali inatumia Shilingi 267,500 kwa kipindi ambacho mtoto anakuwa wodini na wanakaa wastani wa siku 21 kwa ajili ya matibabu.
Mkoko anasema muda wote huo mzazi anatakiwa kujihudumia, anaposhindwa hutokomea na mtoto kusikojulikana na hiyo ndiyo imekuwa changamoto kubwa. Mkoko anasema walipokea watoto 22 wenye ugonjwa wa Utapiamlo kati yao watoto 14 pekee wanatoka kwenye Halmashauri hiyo, wanane walitoka nje ya Halmashauri hiyo ambapo watoto sita wanatoka mkoani Tabora na wawili Mkoani Kagera.
Katibu Tawala Wilaya ya Kahama Glory Absalum anasema si rahisi wananchi hususani wanaotoka maeneo ya vijijini kumudu gharama za kujihudumia wenyewe wakati mtoto akiendelea kupata matibabu kwa muda wote huo. SOMA: DC Mgomi aendelea kuhamasisha lishe bora
Akizungumza kwenye kikao cha robo ya pili ya mwaka kuhusu lishe Glory anasema, “Kwa taarifa iliyopo kwa wilaya hii asilimia 79 ya wazazi, watoto wao waliokuwa wakipata matibabu kwenye hospitali wamekimbia kwa sababu ya kushindwa kumudu gharama,” anasema Absalum.
Glory anasema namna sahihi ya kutatua tatizo hilo ni kuwa na sehemu ya urekebishaji wa afya katika hospitali ya wilaya ambayo utasaidia kupunguza tatizo kwa kiwango kikubwa na wananchi watapunguza gharama za kujihudumia wenyewe kwa serikali kusaidia baadhi ya gharama.
Ofisa lishe kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, Mbuni Chacha anasema kuna aina mbili za utapiamlo ambazo zinawapata watoto ikiwa ambazo ni unyafuzi na kwashakoo na zote zinatibiwa kwa tiba lishe.
Akizungumza na mwandishi wa makala haya katika wiki ya magonjwa yasiyo ambukizwa anasema moja ya sifa ya mtoto mwenye kwashakoo ni kukosa hamu ya kula na mwenye unyafunzi anakuwa ana hamu ya kula sana lakini anakuwa kavimba tumbo na miguu na tiba lishe wanayotumia ni maziwa ya kopo yenye virutubishi.

Chacha anasema maziwa hayo hupatiwa mtoto asiye na hamu ya chakula anapofikishwa hospitalini na humfanya apate hamu baadaye huendelea na tiba lishe maalumu, hatimaye kupata nguvu. Chacha anasema kliniki ya watoto wenye utapiamlo hufanyika siku ya Jumatano na Alhamisi na watoto wenye utapiamlo wengi wao huletwa wakiwa na hali mbaya.
Chacha anasema kwa mwezi mmoja hospitalini hapo wamekuwa wakipokea watoto wanne hadi saba wakiwa na hali ya utapiamlo na kipindi cha kilimo ndiyo kimekuwa hatari zaidi watoto kupata ugonjwa huo. “Kwa nini kipindi cha Masika sababu wazazi wengi hasa maeneo ya vijijini huwaacha nyumbani watoto bila huduma ya chakula kwa muda mrefu wakati mwingine huwapatia chakula cha aina moja pekee,” anasema Chacha.
Chacha anasema mtoto anatakiwa apatiwe vyakula ambavyo ni mlo kamili unaojumuisha vyakula wanga, protini, vitamini na mafuta ili kumuepusha na ugonjwa wa utapiamlo. “Kama atakula vyakula vya wanga pekee nafaka isikobolewe, ale kwa kuchanganya na mboga, matunda kwa wingi kwa ajili ya mmeng’enyo wa mafuta mwili na kulainisha choo na vyakula vya protini,” anasema Chacha.
Chacha anasema mtoto asipopata makundi ya vyakula kwa usahihi ndiyo inakuwa chanzo cha kupata magonjwa yasiyo ambukiza ikiwemo ugonjwa wa utapiamlo ambao mtoto akiupata anatumia gharama kubwa kuutibu.
Kwa mujibu wa aliyekuwa Waziri wa Afya Jenista Mhagama, jumla ya Mashine 230 za kunyunyuzia virutubishi kwenye vyakula zimefungwa katika mikoa 26 nchini na kufikia mashine 1,402 ikilinganishwa na mashine 1,172 zilizokuwepo mwaka 2024.
Katika kutekeleza Mpango Jumuishi wa Pili wa Taifa wa Lishe, Wizara ya Viwanda na Biashara imetoa mafunzo ya kuongeza virutubishi katika vyakula kwa wajasiriamali wadogo na wakati 275 wanaojihusisha na uzalishaji wa unga wa Mahindi katika mikoa sita ya Tanzania Bara.



