Masoud: Ushindi upo mkapige kura

MGOMBEA Urais wa ACT Wazalendo ahitimisha Kampeni Pemba Kwa hamasa na shangwe Mgombea Urais wa ACT Wazalendo Mheshimiwa Othman Masoud Othman, Oktoba 20, 2025 ameanza wiki ya mwisho ya kuhitimisha rasmi kampeni za kuelekea uchaguzi mkuu wa tarehe 29 Oktoba.
Mamia ya wanachama, wapenzi na viongozi wa chama kutoka mikoa yote ya Pemba wamejitokeza kwa wingi kumpokea Othman, mgombea wao. Katika mapokezi hayo yaliyopambwa na nyimbo za uzalendo, ngoma za asili na mabango yenye ujumbe wa matumaini.
Katika mkutano huo viongozi wa ACT Wazalendo walisisitiza kuwa ujio huu wa Mgombea wao ni ishara ya upepo wa ushindi unaovuma kuelekea visiwani vyote vya Zanzibar. SOMA: ACT Wazalendo kudhibiti ufisadi Zanzibar
Safari hii ya Pemba ni ya kipekee kwani inaashiria mwisho wa safari ya kampeni na mwanzo wa safari ya ushindi wa wananchi. ACT Wazalendo inaendelea kusisitiza wito wake kwa wananchi wote kujitokeza kwa wingi kupiga kura kwa amani na kuhakikisha sauti yao inasikika kupitia sanduku la kura.

Mgombea Urais wa ACT Wazalendo, Othman Masoud Othman, amesema hana wasiwasi wowote kuhusu ushindi wa chama chake katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, akisisitiza kuwa tayari ameshaunda timu imara na kuandaa serikali itakayowahudumia Wazanzibari wote bila upendeleo.
Amesema hayo wakati wa uzinduzi wa timu maalumu za vijana wa Othman Masoud (Omo) katika Wilaya ya Chake Chake, Pemba. Othman alisisitiza kuwa chama chake kimefanya kampeni za kipekee, zilizojaa hoja, ukweli na matumaini, na sasa ni wakati wa kuvuna matunda ya kazi kubwa iliyofanywa. Timu hizo za “Omo” zimepewa jukumu maalumu la kulinda ushindi, kuondoa changamoto za maeneo, na kuhakikisha sauti za wananchi zinabaki zinasikika hadi mwisho wa mchakato wa uchaguzi.
Viongozi wa timu hizo ni pamoja na Katibu wa Ngome ya Wanawake Taifa Fatma Alhabib Ferej, Katibu wa Ngome ya Wazee Janetth Fusi, na Katibu wa Ngome ya Vijana Taifa Mohamed Busara, wote wakiahidi kusimama kidete kuhakikisha ushindi wa chama unalindwa kwa umoja, nidhamu na nguvu ya wananchi. Mohamed Busara alisema kuwa safari ya ACT Wazalendo si ya chama pekee, bali ni safari ya kizazi kipya cha wazalendo wanaotaka kuona Zanzibar mpya yenye heshima, fursa na haki kwa wote.
mwisho



