Kilimanjaro waaswa kuacha matumizi mabaya ya fedha

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu.

MKUU wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu amewaasa wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro kuacha matumizi mabaya ya fedha, huku wengine wakiwa na mitambo ya kuiibia Serikali na wananchi.

Babu ametoa maagizo hayo wakati wa kikao na waandishi wa habari na timu ya wataalamu ya utoaji wa elimu ya fedha, katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa iliyofanyika Wilaya ya Moshi Manispaa mkoani humo.

Advertisement

“Kupitia elimu hii ambayo itawafikia makundi mbalimbali itasaidia wananchi kutambua matumizi sahihi ya fedha. Pia nimefurahi kusikia mtafika katika Shule za Msingi na Sekondari; mtawasaidia vijana kwa sababu wapo vijana hawatambui thamani ya fedha,”amesema Babu.

SOMA: Watanzania kupewa elimu ya fedha kuchangia maendeleo

Aidha Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro, Yusuphu Nzowa, ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Fedha kwa kuleta timu hiyo Mkoa wa Kilimanjaro kwani itawafikia wananchi hasa wastaafu ambao baada ya kustaafu wanajikuta wameingia kwenye biashara ambazo hawana taaluma nazo na kuwasababishia hasara.


“Nashukuru kwa ujio huu kuja kutoa elimu hii kwani itawafikia wananchi hasa wastaafu, kwani kumekuwa na kasumba ya wastaafu wengi kujiingiza katika biashara ambazo hawana taaluma nazo baada ya kustaafu hivyo kuwapelekea kupata hasara kubwa,” amesema Nzowa.

Awali akizungumzia madhumuni ya elimu ya fedha, Mkurugenzi Msaidizi kutoka Wizara ya Fedha, Idara ya Uendeshaji wa Sekta ya Fedha, Dionensia Mjema amesema Serikali inataka kuweka uelewa kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya huduma za fedha zinazotolewa nchini ili kujenga uchumi na kuondoa umasikini, Kuinarisha ufanisi wa masoko ya fedha kupitia Elimu ya Fedha na kuongeza upatikanaji wa huduma za fedha.

Ametaja uelewa mwingine watakaoupata wananchi kuwa ni elimu ya kuwezesha kumlinda mtumiaji wa huduma za fedha, kuwezesha wananchi kusimamia vizuri rasilimali fedha, kuwezesha wajasiriamali wadogo kuongeza ujuzi na matumizi sahihi ya huduma za fedha katika kukuza biashara zao, kuimarika kwa utamaduni wa kujiwekea akiba, kukopa na kulipa madeni; na kuongezeka kwa mchango wa Sekta ya Fedha kwenye ukuaji wa Uchumi.

Dionensia amesema kuwa timu ya wataalamu ya utoaji wa elimu ya fedha kwa Mkoa wa Kilimanjaro imelenga kuwafikia wadau mbalimbali wakiwemo wahamasishaji wa biashara ya huduma ndogo za fedha, Vyama vya Ushirika wa Akiba na Mikopo, vikundi vya kijamii vya huduma ndogo za fedha, watoa huduma za fedha na vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalum.

Makundi mengine ni vikundi vya boda boda, machinga, wafanyabiashara, wakulima, watumishi wa umma, wanafunzi, wakufunzi, wajasiriamali wadogo na wa kati, asasi za kiraia, wahariri na waandishi wa vyombo vya habari, watoto na Umma kwa ujumla.

Kwa Mkoa wa Kilimanjaro, Elimu hiyo itatolewa kwa siku kumi na nne (14) katika Wilaya za Moshi Manispaa, Moshi Vijijini, Rombo, Same, Mwanga na Hai.

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *