Kinana akemea ukabila CCM Kigoma

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimekemea udini, ukabila na ukanda kwa wanachama wake wanaowania uongozi na kuagiza mtu wa aina hiyo akatwe mapema, kwani hafai kuchaguliwa.
Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Abdulrahman Kinana ametoa onyo hilo leo Septemba Mosi, 2022 wakati akizungumza na wanachama wa chama hicho katika mkutano wa ndani mjini Kigoma, katika ziara yake ya kukagua utekelezaji wa Ilani, kusikiliza kero, kukagua miradi.
Amesema watu wanaoimba ukabila hawana sifa za uongozi kwa kuwa tangu kuasisiwa chama hicho na viongozi waliotangulia, walikemea mambo hayo wakati wote, hata makabila madogo yamekuwa yakitoa viongozi weledi na wachapa kazi.
“Mwalimu Nyerere alitoka kabila dogo sana, aliongoza nchi hii kwa miaka 24 kwa weledi mkubwa, hakua na ukabila na alikemea siku zote za uhai wake, Hayati Benjamin Mkapa alitoka kabila dogo sana, alikua na uwezo mkubwa na alikemea ukabila kwa nguvu zote
“Chama hiki ni mali ya wote na kiongozi ndani ya chama hiki atachaguliwa kwa sifa, bila kujali anatoka kabila gani, au kanda ipi, jambo la msingi awe ni mtu mwenye uwezo katika kuwaunganisha watu na kuwaletea maendeleo, huyo ndiye anatakiwa,” amesema Kinana na kuongeza:
“Mtu anachaguliwa kwa uwezo wake sio kwa kabila lake, kabila langu hovyo, mvivu, hana jambo jipya mtu kama huyo wa nini?” Alihoji.
Kauli ya Kinana imekuja baada ya Katibu wa CCM Mkoa wa Kigoma, Mobutu Malima awali akiwasilisha taarifa ya uchaguzi wa chama hicho alisema changamoto kubwa waliiyokumbana nayo ni suala la ukabila, kauli iliyoonekana kumkera Kinana.
Katika taarifa yake Mobutu alisema kumeanza kuibuka hisia za ukabila, udini na ukanda katika kutafuta uongozi wa chama ndani ya mkoa huo.
Malima alisema hali hiyo inaweza kukifanya chama kionekana kuwabeba watu wa kabila fulani na kuwatenga wengine, jambo ambalo halitakuwa na afya.
Taarifa hiyo ilionekana kumkera Kinana ambaye alisema: “ Karne hii ya 21 mnahubiri ukabila? Anayehangaika na ukabila hana sifa hata kidogo ya kupigiwa kura, ni lazima muangalie watu wa namna hiyo, ambao hata Hayati Mwalimu Julius Nyerere alishawakataa kuwa hawafai.
“Mkiona vipi mkateni jina lake mapema na mtu aambiwe ukweli, bahati nzuri mwaka huu hatuna ufukara wa wagombea wengi, tuna kazi ya kupunguza watu, siyo kutafuta watu wa kugombea, watu wengi wana mapenzi mema na chama chetu na wanadhamira ya dhati, lakini linapokuja suala la ukabila wanakaa pembeni na tatizo hili linachangiwa na baadhi ya sisi viongozi.
“Hata chaguzi zilizofanyika kama kuna dosari hizi uchaguzi ikiwezekana ufutwe uanze upya, ” amesema.