Kushabikia uvunjifu wa amani ni kujikwamisha wenyewe kimaendeleo

MOJA ya siri kubwa ya maendeleo katika taifa lolote ni utulivu wa kisiasa, kijamii na kiuchumi.

Hata hivyo utulivu huo hauwezi kupatikana kama hakuna amani ndani ya taifa husika, ndio maana viongozi na Watanzania wa makundi mbalimbali wameendelea kusisitizana kuitunza na kuilinda amani.

Waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba akizungumza na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari Novemba 25 alisisitiza tena kila Mtanzania kuomba na kukataa kutokea tena hali ya uvunjifu wa amani iliyotokea katika Uchaguzi Mkuu, Oktoba 29, mwaka huu.

Tukimnukuu alisema, “Sote na kila mmoja kwenye dhamira, aombe jambo la aina hii lisitokee tena, maana si jambo la baraka na linapotokea huacha makovu… Mungu ametupa nchi nzuri Tanzania tuitunze na si mali ya serikali au vyama vya siasa ni nchi yetu sote,” alisisitiza Dk Mwigulu.

Tunaamini kutokana na amani kuwa nguzo kuu inayolibeba taifa lolote linalotamani kupiga hatua katika maendeleo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi ikiwemo Tanzania ndio maana viongozi wameendelea kusihi, kusisitiza na kuwakumbusha Watanzania kuwa makini na kukataa kushawishiwa tena kuruhusu vurugu ndani ya taifa na nchi hii nzuri ambayo tumekuwa nayo.

Tusisahau kuwa amani hiyo imefanya miaka mingi Tanzania imekuwa ikitajwa kama kisiwa cha utulivu katika ukanda wa Afrika Mashariki, sifa ambayo imechangia kuvutia uwekezaji, kukuza utalii na kuwezesha jamii kuishi kwa mshikamano.

Hata hivyo lazima itambulike kuwa hali hii nzuri haiwezi kudumu iwapo baadhi ya Watanzania wataendelea kushabikia au kufumbia macho vitendo vinavyohatarisha amani.

Tunazidi kusisitiza Watanzania kuwa makini na kuepuka hali za aina zozote ile zinazoleta uvunjifu wa amani ikiwa ni pamoja na kuepuka matamshi ya uchochezi, misuguano ya kijamii na tabia za kudharau taasisi za umma bila kujenga hoja zenye tija.

Tusikubali kusombwa na wimbi la matukio ya uchochezi wa vurugu na kuvunja amani yanayoendelea katika mitandao ya kijamii.

Ni dhahiri kuendelea kushabikia mitazamo inayochochea migogoro badala ya mazungumzo ni kuhatarisha amani na kujirudisha nyumba kimaendeleo.

Hivyo rai yetu kwa Watanzania wa makundi na matabaka yote wasikubali kushabikia au kuhalalisha vitendo vya kuvunja sheria na kushiriki kuyumbisha misingi ya taifa letu.

Kama tutayakumbatia haya mambo maovu matokeo yake ni kuporomoka kwa uchumi, kupungua kwa uwekezaji na kusuasua kwa huduma muhimu kama elimu na afya.

Tunaamini Tanzania itapiga hatua zaidi ikiwa kila mwanajamii hatashabikia mambo yanayoturudisha nyuma. Ikumbukwe amani si tu thamani ila ni mtaji wa maendeleo.

Tuiheshimu, tuilinde na tuikemee kila mara tunapoona amani inataka kuhatarishwa.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button