Mgombea ubunge Ngorongoro ahamasisha amani kesho

ARUSHA: Mgombea ubunge wa Jimbo la Ngorongoro kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Yanick Ndoinyo, ametoa wito kwa wananchi wa kata zote 28 za jimbo hilo kuhakikisha wanajitoa kwenda kupiga kura lengo ni kutimiza wajibu wao wa kikatiba.

Akizungumza katika kikao cha kufunga kampeni za CCM ngazi ya Wilaya ya Ngorongoro, kilichofanyika katika kata ya Oldonyo Sambu,Ndoinyo amesema wananchi wa Ngorongoro wanapaswa kuendeleza imani yao kwa CCM kwa kumpigia kura yeye pamoja na madiwani wa chama hicho.

Ndoinyo pia ameeleza kuwa Rais Samia ametuma salamu za upendo na pongezi kwa wananchi wa Ngorongoro, akiwashukuru kwa ushirikiano wao katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo sekta za elimu, afya na miundombinu.

Amesema njia bora ya kuonesha shukrani hizo ni kwa wananchi kuichagua CCM kwa kura za kishindo ili Serikali iendelee kutimiza ahadi zake kwa vitendo.

Kwa upande wake, Massawe Zacharia, Mwenyekiti wa kijiji cha Jema, amesema kuwa Ilani ya CCM imeweka bayana wajibu wa wananchi katika kushiriki maendeleo ya taifa, hivyo ni muhimu wananchi kuunga mkono juhudi hizo kwa kuchagua viongozi wa chama hicho.

Massawe ameongeza kuwa wananchi wa Ngorongoro wameshuhudia maendeleo makubwa katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita kupitia miradi ya maji, afya na elimu, hivyo kuichagua CCM ni kuendeleza mafanikio hayo.

Kikao hicho cha kufunga kampeni kimehudhuriwa na mamia ya wananchi, viongozi wa chama, na wapenzi wa CCM, huku hamasa kubwa ikionekana kuelekea siku ya uchaguzi kwenda kwa wingi kupiga kura.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button