Mmoja afa ajali ya basi, lori Geita

BASI la abiria lenye namba za usajili T.708 DPS, mali ya Kampuni ya Mallessa’s linalofanya safari zake kati ya Geita-Dar es Salaam limepata ajali kwa kugongana uso kwa uso na lori aina ya Mitsubishi Canter lenye namba T.573 DZW.
Ajali hiyo imetokea Oktoba 07, 2025 majira ya saa 8 usiku katika Kitongoji cha Kitongo, Kata ya Butengorumasa, Wilayani Chato na kupelekea kifo cha mtu mmoja na watu kadhaa kujeruhiwa huku hakuna kifo cha abiria wa basi.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Geita, Adamu Maro ametibitisha kutokea ajali hiyo na kueleza lori la mizigo lilikuwa likiendeshwa na Said Ramadhani (23) na basi la abiria lilikuwa likiendeshwa na Charles Mathayo (43).
Maro amesema kuwa kufuatia ajali hiyo, dereva wa Lori aina ya Mitsubishi Canter, Said Ramadhani amefariki dunia na mwili wake umehifadhiwa katika Kituo cha Afya Katoro kwa taratibu za uchunguzi kabla ya hatua za mazishi.

“Abiria wawili, ambao ni Annastazia Yohana (25) na Ismail Omari (34) wote wakazi wa Dar es Salaam walipata majeraha na wanaendelea kupatiwa matibabu katika Kituo cha Afya cha Katoro na abiria wengine wapo salama.
“Chanzo cha ajali ni uzembe wa dereva wa Mitsubishi Canter, alihama upande wake na kwenda upande wa kulia pasipo kuchukua tahadhari au kuzingatia watumiaji wengine wa barabara kisha kuligonga basi”, amesema.



