MOI kutoa matibabu bure kwa wazee Dar

TAASISI ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) imeandaa kambi maalum ya uchunguzi na ushauri wa kitabibu ya siku tatu kwaajili wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam na nje ya Mkoa huo. Kambi hiyo maalum itakayofanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam kuanzia kesho Oktoba 16 hadi 18,2025.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Meneja Uhusiano wa MOI, Patrick Mvungi, huduma zitakazotolewa katika kambi hiyo ni pamoja na uchunguzi na matibabu ya kibingwa na kibobezi katika maeneo ya mifupa, ubongo, mgongo, mishipa ya fahamu, pamoja na huduma za mazoezi tiba na ushauri wa tiba lishe.
Mvungi amesema kuwa kambi hiyo imelenga kuboresha afya za wazee na kuwapatia nafasi ya kupata huduma za kitaalamu kwa urahisi. “Huduma hizo zitakuwa bure kwa wazee wasio na bima ya afya, huku wenye bima wakitumia bima zao kama kawaida,”amesisitizaMvungi.
Aidha, MOI imewahimiza wazee wote kujitokeza kwa wingi katika kambi hiyo ili kuchangamkia fursa hii muhimu ya kuboresha afya zao. SOMA: Tanzania yahudumia zaidi ya 900 moyo, mifupa Zambia



