Mwinyi: Awamu ijayo ni ya vijana

MGOMBEA urais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hussein Ali Mwinyi, amesema vijana wana nafasi kubwa katika kufanya maamuzi ya taifa na ameahidi kuwapa nafasi zaidi za uongozi katika awamu ijayo.

Akizungumza na makundi mbalimbali ya vijana wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) kutoka vyuo na vyuo vikuu, katika mkutano uliofanyika Chuo cha Vijana cha CCM Tunguu, Mkoa wa Kusini Unguja, Mwinyi alisema CCM itaendelea kuwapa kipaumbele vijana katika masuala ya ajira, elimu na uongozi.

Alisema serikali imeongeza bajeti ya elimu kutoka shilingi bilioni 80 hadi bilioni 864, ikiwa ni sehemu ya dhamira ya kuhakikisha vijana wanapata elimu bora na kuchangia maendeleo ya taifa. Mwinyi alisema serikali itaendelea kujenga vyuo vya elimu ya amali katika kila mkoa ili kuwawezesha vijana kupata ujuzi wa ufundi na kujiajiri.

Aidha, alitangaza mpango wa kuongeza ajira mpya 350,000, akiahidi kuvuka lengo hilo ili kuhakikisha vijana wengi zaidi wananufaika, hususan katika sekta za elimu, afya, vikosi na viwanda. Aliongeza kuwa serikali inaendelea kuboresha miundombinu katika maeneo ya Dunga, Zuze na Pangatupu ili kuimarisha ajira. “Wakati huu ni wa vijana kwa sababu wana elimu, uwezo na ari ya kuijenga Zanzibar,” alisema Mwinyi.

Alisema serikali pia itahamasisha ajira kupitia sekta binafsi na kuongeza mikopo kwa vijana ili waweze kujiajiri, sambamba na kutoa kipaumbele cha ajira kwa vijana wa Kitanzania. Vilevile, aliahidi kuimarisha jumuiya za CCM kwa kujenga ofisi na kumbi za mikutano ili kuboresha shughuli za kijamii na kiuchumi.

Akijibu hoja za vijana, Mwinyi aliahidi kuongeza posho kwa wanafunzi wa elimu ya juu kutokana na ongezeko la mahitaji na changamoto wanazokabiliana nazo. SOMA: NCCR Mageuzi yahimiza amani, yahadharisha vurugu

Kwa kuunga mkono ubunifu, alisema serikali katika awamu ijayo itaanzisha Wizara ya Mawasiliano na Ubunifu kwa lengo la kuendeleza miradi ya ubunifu inayotokana na vyuo na kusaidia taifa kuelekea kwenye uchumi wa kisasa. Mwinyi aliwataka vijana kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura na kumpa kura ili aweze kutekeleza kwa vitendo ahadi zote alizozitoa.

 

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button