Mzumbe wazindua chanjo homa ya ini

MOROGORO: CHUO Kikuu Mzumbe kilichopo mkoani Morogoro kimezindua kampeni ya utoaji chanjo ya homa ya ini (Hepatitis B) kwa watumishi wake wa kampasi zote, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kulinda afya na ustawi wa rasilimali watu ndani ya taasisi hiyo ya elimu ya juu nchini.
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu hicho, Profesa William Mwegoha amesema hayo wakati akizundua kampeni hiyo chuoni hapo.
Amesema chanjo hiyo inayolenga kuwakinga watumishi dhidi ya ugonjwa wa homa ya ini ambao ni miongoni mwa magonjwa hatarishi yanayosababisha vifo vingi duniani.
Profesa Mwegoha amesema hatua hiyo ni sehemu ya mpango mkakati na endelevu wa chuo katika kuhakikisha afya ya watumishi inabaki kuwa ni cha kipaumbele, licha ya kuboresha mazingira ya kazi na ujifunzaji.
“fya ni utajiri bila afya njema huwezi kufanikisha malengo ya kazi wala maendeleo ya chuo na hata shughuli binafsi, hivyo Chuo kinatambua thamani ya rasilimali watu, ndiyo maana tumeamua kuanzisha mpango huu wa chanjo,” amesema Profesa Mwegoha.

“Homa ya ini ni ugonjwa hatari unaoweza kuathiri maisha na uzalishaji kazini, nasisitiza watumishi wote wachukue hatua hii muhimu kwa sababu chuo kimegharamia chanjo kwa watumishi wote,” amesema.
Naye Mkurugenzi wa Afya na Huduma za Kitabibu wa Chuo Kikuu hicho, Dk Nyangara Mtilly, amesema kuwa zoezi la kupata chanjo linafuata utaratibu wa kupima afya kwanza kabla ya mtu kupata chanjo.
Dk Nyangara amesema Chanjo ya Hepatitis B hutolewa kwa watu wazima kwa awamu tatu ili kuhakikisha kinga kamili, wakati watoto wachanga wakipatiwa chanjo mara tu baada ya kuzaliwa.
Naye Mtaalamu wa Kituo cha Afya Chuo Kikuu Mzumbe, Dk Mohamed Ayub, amefafanua kwa undani maana ya ugonjwa wa Homa ya Ini, na aina zake, vyanzo vya maambukizi na namna unavyoweza kuzuilika.
Dk Ayub amesema ni umuhimu kufanya uchunguzi wa mapema ili kuchukua tahadhari za ugonjwa huo ikiwa na kupata chanjo kama njia salama ya kinga na upatikanaji wa tiba kwa waliothirika.
Nao baadhi ya watumishi wa chuo Kikuu hicho kwa nyakati tofauti akiwemo Tekla Francis aliyepata chanjo hiyo ameushukuru uongozi wa chuo kwa kuanzisha mpango huo kwani utasaidia kulinda afya zao na kuongeza ufanisi kazini.
“Tunampongeza uongozi wa chuo kwa kutuleta huduma hii hapa kazini. Wengi tulikuwa hatujui madhara ya ugonjwa huu, lakini sasa tumeelimishwa na tumepewa kinga,” amesema.



