Ndejembi ataka kasi utafutaji gesi, mafuta
Mhandisi Sangweni aliahidi kuwa PURA itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi ili kufikia malengo ya kisekta na kuchangia katika Dira 2050.

DAR ES SALAAM: Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi ameitaka Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kubuni mikakati thabiti itakayosaidia kuongeza kasi ya utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini.
Ndejembi ameyasema hayo jijini Dar es Salaam, Jumatatu (Novemba 24, 2025), baada ya kukutana na menejimenti PURA, ikiwa ni mara ya kwanza tangu apate wadhifa huo.
Katika kikao hicho, Ndejembi alisema kuwa anatarajia kuona PURA inaweka nguvu katika kuandaa na kutekeleza mikakati itakayoongeza kasi ya utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini kwa kuwa tafiti hizo zinachukua muda mrefu.
“Ninatarajia kuona PURA inaandaa na kutekeleza mikakati itakayochagiza utafutaji wa mafuta na gesi asilia katika vitalu mbalimbali vikiwemo Ruvu, Mkuranga na Tanga ambayo itaeleza kwa kina nini kifanyike ili tuweze kupata matokeo tarajiwa,” alisema Ndejembi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Chamawino, Dodoma.
SOMA: PURA yaweka msisitizo elimu miradi kwa wananchi
Sanjari na hilo, Ndejembi aliitaka PURA kuendelea kutoa ushauri wenye tija kwa Wizara kuhusu namna ya kufanya mazingira ya uwekezaji katika mkondo wa juu wa petroli kuwa shindani ili nchi inapokwenda kwenye duru ya tano ya kunadi vitalu vya utafutaji wa mafuta na gesi asilia (5th licencing round) matokeo tarajiwa yapatikane.
“Kabla ya kwenda kwenye duru ya tano ya kunadi vitalu natarajia kuona PURA inatushauri Wizara kuhusu nini hatua za kufuata ili tufanye mazingira yawe rafiki kwa wawekezaji tunaowatarajia huku tukilinda maslahi ya nchi yetu. Nanatarajia ushauri huo uje haraka ili tuweze kuufanikisha” alisistiza Ndejembi.
Ndjejembi pia aliweka bayana kuwa kufanikisha duru ya tano ya kunadi vitalu si tu kutaongeza mapato kwa Serikali lakini kama Wizara itakuwa imeiwezesha Serikali kuacha alama chanya katika sekta.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa PURA Mhandisi Charles Sangweni kwa niaba ya menejimenti ya PURA alimshukuru Waziri Ndejembi na uongozi mzima wa Wizara kwa kutenga muda wao kufanya kikao na menejimenti ya PURA.
Aidha, Sangweni aliahidi kuwa PURA itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi ili kufikia malengo ya kisekta na kuchangia katika Dira 2050.



