Rais Mwinyi: Tuilinde Amani Yetu

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema kudumisha amani ni jukumu la kila mwananchi anayependa maendeleo ya nchi. Dk. Mwinyi aliyasema hayo jana aliposhiriki Sala ya Ijumaa na Dua Maalum ya kuiombea nchi pamoja na Uchaguzi Mkuu, iliyofanyika katika Msikiti wa Muembe Shauri, Mkoa wa Mjini Magharibi.
Amesema kuwa jukumu la kulinda na kudumisha amani si la mtu mmoja pekee, bali ni wajibu wa kila mwananchi kuhakikisha utulivu na mshikamano vinaendelea kuwepo katika nafasi yake. “Amani ndiyo nguzo kuu ya umoja na maendeleo katika sekta zote. Kila mmoja wetu ana wajibu wa kuilinda, kuienzi na kuihubiri, hasa katika kipindi hiki kuelekea Uchaguzi Mkuu,” alisema Dk. Mwinyi.

Rais Mwinyi aliongeza kuwa maendeleo makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha miaka minne iliyopita yametokana na hali ya amani na utulivu, hali iliyowezesha Serikali kutekeleza mipango yake kwa ufanisi. SOMA: Tumezima mwenge tumuenzi Nyerere
Aidha, aliwakumbusha wananchi kuwa maneno au vitendo vya mtu vinaweza kusababisha uvunjifu wa amani, hivyo kila mmoja anatakiwa kuchunga kauli na matendo yake. “Vurugu katika nchi hazianzi kwa bunduki, bali kwa maneno au matendo madogo ambayo baadaye husababisha migogoro na machafuko,” alisema.
Rais Mwinyi amehimiza wananchi kuendeleza hali ya utulivu kabla, wakati na baada ya uchaguzi, sambamba na kufuata maelekezo ya Tume ya Uchaguzi siku ya kupiga kura, ili demokrasia ichukue nafasi yake ipasavyo. Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar unatarajiwa kufanyika tarehe 29 Oktoba 2025.



