Samia ametimiza ndoto za baba wa taifa

KATIBU wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenani Kihongosi amesema kuwa mgombea urais wa Tanzania kupitia chama hicho Dk Samia Suluhu Hassan ametimiza ndoto kubwa mbili za Hayati Baba wa Taifa Mwl. Julius Kambarage Nyerere.
Akizungumza leo Oktoba 10, wakati wa mkutano wa mgombea huyo wilayani Butiama, mwenezi amesema ndoto kubwa ya kwanza ya Baba wa Taifa ilikuwa kujenga mradi mkubwa wa bwawa la kufua umeme ambapo Dk Samia ameitekeleza ndoto hiyo kwa kutekeleza mradi huo wenye uwezo wa kuzalisha megawati 2,115 za umeme na kuongeza uzalishaji wa umeme nchini.
Akizungumzia umuhimu wa mradi huo amesema umelenga kupunguza utegemezi wa umeme kutoka vyanzo vya nje na kuboresha huduma za umeme kwa wananchi. SOMA: Samia: Tunamuenzi baba wa Taifa kwa utawala bora
Aidha, Kihongosi amesema ndoto nyingine ya hayati baba wa taifa ilikuwa ni makao makuu ya Serikali kuhamia mji mkuu wa Tanzania ambao ni Dodoma na kueleza kuwa ndoto hiyo imekamilishwa kwa mihimili yote mitatu ya Serikali, Bunge na Mahakama.
Ameeleza kuwa Dk Samia amekuwa akiyaishi maono ya Baba wa Taifa kwa vitendo na anastahili kuendelea kuaminiwa na kupewa kura nyingi katika uchaguzi mkuu ujao.



