Serikali yaingiza bil 1/- zao la utomvu

KILIMANJARO: SERIKALI imeanza kunufaika na mapato ya zao jipya linalotokana na mti aina ya msindano kisayansi ukijulikana jina la “ Pinus patula au pine tree” yanayofikia Sh bilioni 1 kutokana na ugemaji wa utomvu kupitia mashamba ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Kaskazini .
Kamishna Msaidizi Mwandamizi (SACC) James Nshare amesema hayo mjini Same alipoelezea mkakati wa uendelezaji uhifadhi misitu, utalii ikolojia na mafanikio ya Wakala katika kanda hiyo kwenye uchangiaji wa pato ya taifa.

Nshare ambaye pia ni Kamanda wa Kanda ya Kaskazini inayojumisha mikoa ya Tanga, Kilimanjao na Arusha, aliyataja mashamba hayo ni Meru, West Kilimanjaro na Rongai North Kilimanjaro ambapo kwa sasa ugemaji wa utomvu unaendelea.
Alisema kanda hiyo ina idadi ya mashamba sita ukilinganisha na kanda zingine kwa idadi na si kwa ukubwa na yanatoa fursa mbalimbali za utalii ikiwemo la kuanzisha zao hilo jipya la ugemaji wa utomvu au resin.
“Utomvu ni moja wapo ya zao jipya ambalo limeazishwa na linaingiza fedha nyingi, kinachofanyika utomvu unagemwa na mti uinaendelea kuweza kuishi kwa ajili ya matumzi mengine ya mti mbao, utomvu unagemwa na mti inaendelea kuweza kuishi,”alisema Nshare.

Nshare alisema biashara hiyi imekuwa ni lulu na wawekezaji wengi kutoka nje ya nchi wanakuja kuwekeza kwa ajili ya shughuli za ugemaji wa utomvu na kusafirishwa kwenda nje ya nchi na kuliingizia Taifa fedha nyingi.
Alisema utomvu una matumizi mengi ikiwemo kutengeneza mpira ,magurudumu, gloves na bidhaa nyingine za viwandani.
Alisema kwa sasa mkakati wa Serikali kwa ni kuona shughuli za uchakataji unafanyika hapa nchini ili kuongeza thamani kwa lengo la kuongeza ajira kwa ajili ya Watanzania na bidhaa hiyo iweza kupatikana hapa nchini.
“Mtanzamo wa serikali ni kuita zaidi wawekezaji waje kuwekeza kwenye viwanda huku ikiendelea kuongeza wataalam ambapo Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeazisha mtaala wa Uzamivu wa masuala ya utomvu,” alisema Nshare.
Nshare alisema kutokana na kuwepo kwa mtaala huo kutawezesha kuongeza wataalam ambao watakuwa hapa nchini kwa ajili ya kutoa utaalamu badala ya kutengemea kutoka nje ya nchi.
Alisema pia katika Chuo Cha Misitu Olmotonyi pamoja Forest Industries Training Institute (FITI) ambapo kwa sasa vimelipa kipaumbele ili kulisaidia Taifa kupata wataalamu ili baadaye kupanua wigo wa mapato ya serikali kupitia zao la utomvu.
“Tunakaribisha watu kuja kuwekeza na ni fursa nyingine kwa mashamba yetu tuliyokuwa nayo katika kanda ya Kaskazini,” alisema Nshare.
Kwa upande wake Mhifadhi Mwandamizi wa TFS Shamba la Miti Norh Kilimanjaro,Fred Ng’wavi alisema kuwa mwaka wa fedha 2025/2026 ilikadiriwa kuvuna kilogramu 600,000 za utomvu.
Ng’wavi alisema ugemaji wa utomvu una takribani miezi 11 iliyopita na tayari zimevunwa kilogramu 300,638 kufikia mwishoni mwa Aprili 2026 na kuingiza pato sawa na fedha Sh milioni 178,978.
Alisema shamba hilo lilianzishwa mwaka 1926 lina ukubwa wa hekta 8,609 na limegawanyika kwenye safu sita ambazo ni Endoneti, Rongai, Kamwanga, Nalemoru, Nanjala, Tarakea.



