Mwinyi atangaza mkakati mpya sekta ya afya

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) inatarajia kujenga hospitali mbili kubwa za rufaa zitakazotoa huduma za kibingwa kwa maradhi ya moyo, saratani, ubongo na uti wa mgongo.

Akizungumza Ikulu Zanzibar jana, wakati wa hafla ya utiaji saini wa mkataba wa ujenzi, ukarabati na upanuzi wa Hospitali ya Mnazi Mmoja kati ya SMZ na Kampuni ya Jiangxi International Economic and Technical Cooperation Co. Limited, Dk. Mwinyi alisema hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za serikali kuboresha huduma za afya nchini.

Katika hafla hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dk. Mngereza Miraji Mzee, alisaini kwa niaba ya Serikali ya Zanzibar, huku Mkurugenzi wa Kampuni ya Jiangxi International, Bw. Peng Chao, akisaini kwa niaba ya kampuni hiyo.

Dk. Mwinyi alisema tukio hilo linaashiria dhamira ya serikali kuhakikisha huduma bora za afya zinapatikana nchini, akisisitiza kuwa Hospitali ya Mnazi Mmoja itabadilishwa na kuwa hospitali ya kisasa yenye miundombinu na vifaa vya kisasa vya tiba.

Amesema sekta ya afya ina mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa kwa kuwa wananchi wenye afya bora ndio msingi wa uchumi imara na ustawi wa jamii. SOMA: ACT Wazalendo: Afya bure 100% ikishinda

Rais Mwinyi alieleza kuwa baada ya serikali kukamilisha ujenzi wa hospitali katika ngazi ya msingi, wilaya na mkoa, hatua inayofuata ni kujenga hospitali tano za rufaa – moja katika kila mkoa – zitakazotoa huduma za kisasa zenye viwango vya kimataifa.

Alizitaja hospitali mbili zitakazoongezwa kujengwa ni  hospitali ya Matibabu ya Magonjwa ya Saratani, Moyo na Mifupa, na Hospitali ya Rufaa na Kufundishia Watendaji wa Sekta ya Afya, itakayojengwa Binguni.

Dk. Mwinyi alisema kukamilika kwa hospitali hizo kutawezesha Zanzibar kuachana na utaratibu wa kusafirisha wagonjwa nje ya nchi, kwani huduma za matibabu ya kibingwa zitapatikana nchini kwa ubora unaokubalika kimataifa.

Akizungumzia mradi wa Hospitali ya Mnazi Mmoja, Rais Mwinyi alisema sekta ya afya inaandika historia mpya na akaipongeza Wizara ya Afya pamoja na watendaji wote waliofanikisha kukamilika kwa mkataba wa mradi huo. Aidha, aliagiza Wizara ya Afya kusimamia kwa karibu kampuni ya ujenzi ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati na kwa ubora uliokubaliwa.

Mradi wa ujenzi wa Hospitali ya Mnazi Mmoja unatekelezwa chini ya ufadhili wa Benki ya BADEA, Kuwait Fund na Saudi Fund, kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, na unatarajiwa kukamilika ifikapo Juni 2027.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button