Tanzania yaandaa tuzo za utalii Duniani

DAR-ES-SALAAM : TANZANIA imeandika historia kwa kuwa mwenyeji wa hafla ya Tuzo za 32 za Utalii Duniani (World Travel Awards) kwa ukanda wa Afrika na Bahari ya Hindi, tukio ambalo linafanyika kwa mara ya kwanza nchini tangu kuanzishwa kwa tuzo hizo mwaka 1993.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika usiku huu katika Hoteli ya Johari Rotana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Ephraim Mafuru, alitoa salamu za ukaribisho kwa wageni wa ndani na nje ya nchi waliohudhuria tukio hilo kubwa la kimataifa.

“Tanzania imepata heshima ya kipekee kuwa mwenyeji wa hafla hii ya kihistoria, jambo linalothibitisha ukuaji wa sekta ya utalii na nafasi yetu katika ramani ya utalii duniani,” alisema Mafuru.

 

Tuzo hizi, ambazo hutolewa kwa kutambua ubora na ubunifu katika sekta ya utalii, zimekusanya wadau kutoka mataifa mbalimbali, wakiwemo watoa huduma za utalii, hoteli, mashirika ya ndege, na mamlaka za utalii kutoka Afrika na eneo la Bahari ya Hindi.

Kwa mara ya kwanza, Tanzania imepewa nafasi ya kuonesha vivutio vyake vya kipekee mbele ya wadau wakubwa wa sekta hiyo, ikiwa ni pamoja na fursa za uwekezaji, utamaduni, na urithi wa asili unaovutia wageni kutoka pande zote za dunia.

Hafla hii pia inatazamwa kama jukwaa muhimu la kutangaza vivutio vya ndani, kuimarisha uhusiano wa kimataifa, na kuvutia wawekezaji katika sekta ya utalii inayochangia kwa kiasi kikubwa katika pato la taifa.

SOMA: AviaDev Afrika 2025: Mafanikio makubwa usafiri wa anga, utalii

 

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button