Vijana Kigoma wafunguka kuelekea Oktoba 29

KIGOMA; KUELEKEA uchaguzi Mkuu wa Rais, wabunge na madiwani Oktoba 29, vijana mkoani Kigoma wamewataka vijana wenzao kujitokeza kwa wingi kushiriki katika zoezi hilo kwa kuwachagua viongozi wanaowataka badala ya kujiingiza kwenye mambo ambayo yanaweza kuchagia vurugu wakati wa zoezi hilo.
Vijana hao wametoa kauli hiyo wakati wa mbio za taratibu ‘jogging’ zilizojumuisha vikundi mbalimbali vya jogging vya mjini Kigoma zoezi lililoenda sambamba na kufanya kufanya usafi katika maeneo mbalimbali ya Manispaa ya Kigoma Ujiji.
Mmoja wa vijana hao, Mzee Saliboko alisema kuwa kupiga kura ndiyo msingi wa maendeleo kwani inawapa wananchi nafasi ya kuchagua viongozi wanaowataka na kuachana na viongozi ambao hawakutimiza wajibu wao katika kuwatumikia wananchi au kuwachagua tena waliofanya vizuri na kwamba kususia kupiga kura au kushiriki vurugu kunawanyima fursa ya kuchagua watu wengi.

Naye, Asia Salum kijana mwingine aliyeshiriki jogging hiyo kutoka kata ya Kitongoni Ujiji Mjini Kigoma alisema kuwa vijana wa Kigoma wamepambana katika kuvifanyia kampeni vyama vyao hivyo vijana wengi wana mwamko wa kujitokeza kupiga kura ili kuona waliowapigania wanapata ushindi na vijana wengi hawako tayari kushiriki vurugu au kukosa kupiga kura.

Kwa upande wake kiongozi wa Jogging ya Kitongoni Ujiji mjini Kigoma, Abdallah Seif alisema kuwa vijana wengi wa Kigoma wana mwamko Mkubwa wa siasa na wanajua wanachokisimamia hivyo hawako tayari kushiriki kwenye mambo ambayo hayana manufaa kwao ikiwemo kuzuia uchaguzi hasa upigaji kura kwa kushiriki maandamano Oktoba 29 na kwamba vikundi vya jogging vimehamasika kushiriki zoezi la upigaji.
Akipokea jogging hizo na baadaye kushiriki kwenye zoezi la usafi Mkuu wa Mkoa Kigoma, Balozi Simon Sirro amewataka vijana kutumia haki yao ya kikatiba ya kujitokeza kwa wingi kupiga kura kuchagua viongozi wanaowaamini kuwa watawaletea maendeleo.




