Viongozi wa dini, waandishi watakiwa kuhimiza amani uchaguzi mkuu

IRINGA: Waandishi wa habari na viongozi wa dini wametakiwa kutumia nafasi zao kuhimiza amani na umoja wa kitaifa, hususan katika kipindi hiki kinachoelekea uchaguzi mkuu, ili kuepusha mifarakano na migawanyiko miongoni mwa Watanzania.

Kauli hiyo imetolewa mjini Iringa katika warsha ya siku moja iliyoratibiwa na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) kwa kushirikisha waandishi wa habari na viongozi wa dini kutoka madhehebu mbalimbali.

Mwezeshaji wa semina hiyo, Uzima Justine, alisema huu ni wakati sahihi kwa viongozi wa dini kutoa ujumbe unaowaunganisha Watanzania, badala ya maneno yanayoweza kuchochea chuki au migawanyiko.

“Chochote kisichounganisha watu na kuleta amani si cha kweli,” alisema Uzima, akisisitiza kwamba wajibu wa viongozi wa dini ni kujenga maridhiano na upendo wakati wote, hasa katika kipindi cha uchaguzi.

Kwa upande wake, Mratibu wa warsha hiyo, Omary Ibrahim, ambaye ni Afisa Miradi wa BAKWATA Makao Makuu, alisema warsha hiyo imelenga kuwaongezea uelewa washiriki kuhusu nafasi yao muhimu katika kulinda amani kupitia maneno na matendo yao.

“Tupo Iringa na tumewakutanisha waandishi wa habari pamoja na viongozi wa dini — watu ambao wanaweza kujenga au kubomoa. Lengo letu ni kuwajengea uwezo ili wakatoe elimu sahihi kwa wananchi, wasitoke nje ya misingi ya ukweli,” alisema Omary.

Aliongeza kuwa wakati mwingine haki ya kukusanya, kuchakata na kusambaza habari haitumiki ipasavyo, jambo linaloweza kuleta mkanganyiko kwa jamii na kuhatarisha amani ya nchi.

Ustadh Othman Sabuni, mmoja wa washiriki wa warsha hiyo, alisema kudumisha amani kunapaswa kuanzia kwenye majukwaa ya dini, kwani mafundisho yenye busara na yasiyoegemea upande wowote yana mchango mkubwa katika kuimarisha utulivu wa taifa.

“Kudumisha amani inapokuwa sehemu ya mafundisho yetu ni muhimu sana. Vivyo hivyo, waandishi wa habari wanapaswa kuhakikisha hawapotoshi ukweli, kwa sababu habari sahihi ni silaha ya kulinda amani,” alisema.

Naye Mchungaji Judith Sanga wa kanisa la Glory to God Miracle Mission Tanzania, alisema amani si tu kukosekana kwa vita, bali ni maisha ya kila siku ya mtu — kuishi kwa utulivu, kuhurumiana na kuheshimiana.

“Kila kiongozi wa dini ana wajibu wa kuipandikiza amani katika mioyo ya waumini wake, na kila mwandishi ana jukumu la kuandika ukweli unaojenga taifa,” alisema Mchungaji Sanga.

Katika warsha hiyo wito umetolewa kwa taasisi za dini na vyombo vya habari kushirikiana kwa karibu zaidi katika kutoa elimu ya uraia, kueleza kwa uwazi umuhimu wa amani, na kupinga taarifa au mafundisho yanayoweza kugawa jamii.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button