Wagonjwa wa figo waongezeka Temeke

DAR –ES –SALAAM : IMEELEZWA kuwa idadi ya wagonjwa wa figo inazidi kuongezeka hapa nchini ukilinganisha na hapo awali ambapo wagonjwa walikuwa wachache lakini sasa idadi ya wagonjwa inazidi kuongezeka.
Akizungumzia kuhusu ukubwa wa tatizo hilo hilo jijini DSM, katika mahojiano maalum na Dailynews Digital, Daktari wa kitengo cha usafishaji damu Hospitali ya Rufaa ya Temeke Dk. Grace Mhagama amesema visababishi vikubwa vinavyochangia mtu kupata ugonjwa wa figo ni mtindo wa maisha wa ulaji wa vyakula, unywaji wa dawa kiholela bila ya ushauri wa daktari na watu wengi kushindwa kufuatilia afya zao mapema.
“ matumizi mabaya ya dawa ama tiba mbadala anajiamulia kunywa bila ya ushauri wa daktari wengine wanaenda pharmacy wanajinunulia dawa hafiki hospitali lakini hajui madhara yake baadaye ”, amesema Dk.Mhagama.
Hivi sasa katika Hospitali ya Rufaa ya Temeke ina idadi ya wagonjwa 32 ambao wanapatiwa tiba ya usafishaji wa damu kitaalamu inaitwa (Dialysis).
Dk. Mhagama ameishukuru serikali kwa kuingiza matibabu ya ugonjwa huu katika huduma za bima ya afya ambapo sasa watanzania wengi wenye changamoto za figo wanatibiwa kupitia bima ya afya na kupewa ushauri bila ya uwoga wa gharama za tiba.
“ Tunaishukuru serikali tumepata kibali cha kuwahudumia wagonjwa wa bima ya afya na sasa tunawagonjwa wa NHIF tunashukuru sana ,” Alimalizia.



