WAKULIMA wilayani Hanang wamepewa mafunzo yanayolenga kuhimiza matumizi ya zana za kisasa za kilimo na utunzaji wa kumbukumbu za matumizi ya fedha.
Mafunzo hayo yameandaliwa na taasisi ya EFTA kwa kushirikiana na Benki ya CRDB pamoja na wazalishaji na wauzaji wa matrekta ya New Holland kupitia kampuni ya Hughes Agriculture Tanzania, yenye lengo la kuhakikisha wakulima nchini wanalima kwa kutumia zana za kilimo za kisasa.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo ya kwanza kwa wakulima wa Hanang katika mji wa Katesh, Mkuu wa Wilaya ya Hanang, Janeth Mayanja, amesema ili wakulima waweze kulima kwa ufanisi ni lazima serikali kwa kushirikiana na taasisi binafsi zitengeneze mazingira rafiki yatakayowezesha mkulima kuziona fursa mbele yake.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa EFTA, Nicomed Bohay amesema sambamba na mafunzo juu ya matumizi ya mashine katika kilimo, taasisi yake imewaletea mikopo ya mashine hasa matrekta ya New Holland, ambayo yatakuwa yakipatikana kwa mkopo kwa wakulima bila dhamana.