Walimu Gairo, Kisarawe, Ludewa wanufaika mbinu ufundishaji KKK

MOROGORO: WALIMU zaidi ya 200  kutoka shule za msingi katika wilaya tatu za mikoa ya Pwani, Njombe na Morogoro wamejengewa uwezo wa  kutumia  mbinu rafiki za ufundishaji wa stadi za kusoma , kuandika na kuhesabu (KKK) kwa wanafunzi kupitia  Mradi wa ‘Kijiji Changu’ uliotekelezwa na   Shirika lisilo la Kiserikali  Uwezo Tanzania.

Meneja wa Mawasiliano wa Shirika hilo , Greyson Mgoi amesema hayo  mjini Morogoro kwenye mkutano wa kutathimini utekelezaji wa mradi na kushirikisha  baadhi ya walimu , Maofisa Elimu ya Awali na Msingi  wa Wilaya ya Gairo, mkoani Morogoro, Kisarawe mkoani Pwani na Ludewa katika Mkoa wa Njombe.

Mgoi amesema mradi huo licha ya kuwajengea uwezo walimu  pia umewafikia wanafunzi zaidi ya 7,000  katika shule zilizopo  kwenye vijiji  100 vilivyopo katika   wilaya hizo.

Advertisement

Amesema Shirika hilo linatekeleza jitihada mbalimbali  zinazolenga kusaidia watoto kupata kujifunza, kuchangia katika ubora wa elimu kwa kushirikiana na wadau  kuboresha elimu na sera.

Mgoi amesema  utekelezaji wa mradi huo  ulianza  mwaka 2022 na umefikia tamati  Desemba mwaka jana (2023),na  ulilenga kupunguza changamoto  za  wanafunzi wanaoshindwa kumudu vyema stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu  kwa baadhi ya wanafunzi wa  wilaya  hizo.

Amesema  kabla ya kuanza mradi maeneo hayo wanafunzi walipimwa walionekana kushindwa kumudu vyema stadi hizo , lakini kwa sasa wameongeza uwezo wa  ufauli wa kusoma , kuandika na kuhesabu.