Wasira asifu uhodari, uwezo wa Dk Samia

MARA: MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira, amemtaja mgombea urais wa Tanzania kupitia chama hicho, Dk Samia Suluhu Hassan, kama kiongozi hodari na mzoefu katika uongozi.

Kauli hiyo ameitoa leo, Oktoba 9, 2025, alipokuwa akihutubia wananchi wa Bunda mkoani Mara, wakati wa kampeni za mgombea huyo. Wasira alisisitiza kuwa upole, hekima, na tafakari za Dk Samia zimewezesha kutekeleza majukumu yake kwa mafanikio makubwa kwa muda mfupi.

Aidha, amemsihi Dk Samia kutobabaishwa na kile alichokiita “chokochoko za mtandaoni,” huku akisema ni mambo yanayotokana na watu wachache wanaotumia mitandao ya kijamii kwa malengo yasiyo mema.

Wasira pia amekumbusha changamoto alizokumbana nazo Dk Samia alipokuwa akichukua madaraka mwaka 2021, kufuatia kifo cha mtangulizi wake, Rais wa Awamu ya Tano, hayati John Pombe Magufuli, pamoja na kuibuka kwa janga la ugonjwa wa virusi vya corona.

 

“Wakati huo, Dk Samia alituambia maneno mawili tu, ‘Kazi iendelee.’ Miaka minne baadaye, kazi imeendelea licha ya mazingira magumu. Dk Samia ameongoza nchi yetu kwa kuhakikisha umoja na amani vinaendelea kuwepo nchini.

“Zipo chokochoko nyingi mtandaoni, lakini ni watu wachache sana wanaotumia mitandao hiyo kwa malengo ya kuleta machafuko. Naomba msome mitandao kwa uangalifu, maana kuna watu wachache ambao hawaridhiki.

“Kwa wale mnaopika maharage mnaelewa, kuna maharage hayaivi kabisa yanabaki madogo na kuonekana juu. Hawa ndio wanaosumbua kwenye mitandao, lakini hawawezi kuisumbua nchi yetu,” amesema Wasira.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button