Watashauriwa kuwajibika kukabili usugu wa dawa

MWANZA: WAFAMASIA nchini wametakiwa kuchukua hatua za haraka kukabiliana na ongezeka sugu la vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa, kwa kutoa elimu sahihi kwa wananchi kuhusu matumizi bora na salama ya dawa.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda ametoa kauli hiyo Novemba 26, 2025, katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wateknolojia Dawa na Wateknolojia Dawa Wasaidizi Tanzania (TAPHATA) uliofanyika jijini Mwanza.
Mtanda amesema endapo hatua stahiki hazitachukuliwa dhidi ya usugu wa vimelea vya magonjwa, dunia inaweza kukumbwa na vifo vya zaidi ya watu milioni 10 kila mwaka ifikapo 2050, kama ilivyoainishwa kwenye ripoti ya Benki ya Dunia ya mwaka 2018.

“Hakikisheni mnatoa elimu sahihi kwa wananchi juu ya matumizi sahihi ya dawa kwa kuwa ninyi ndiyo kada ya afya inayohusika zaidi,”alisema Mtanda.
Aidha, Mkuu wa Mkoa amezitaka mamlaka na mabaraza yanayohusika na usimamizi wa dawa kuhakikisha maduka yote ya dawa nchini yanasajiliwa na kukaguliwa mara kwa mara. Pia amesisitiza umuhimu wa vituo vya afya vya umma na binafsi kuwa na mtaalamu stahiki wa dawa kwa mujibu wa viwango na ikama ya wizara.
Akizungumzia changamoto zinazowakabili wataalamu hao, Mtanda amesema bado kuna suala la upungufu wa ajira, maslahi madogo katika sekta binafsi na changamoto za usimamizi wa maduka ya dawa.
“Nitoe wito kwa Baraza la Famasi na Ofisi ya Mfamasia Mkuu wa Serikali kushirikiana kwa karibu na chama chenu ili kusikiliza na kushughulikia changamoto hizi, ili taaluma hii iwe na nguvu zaidi na tija kwa taifa,”alisisitiza.

Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kuimarisha rasilimali watu katika sekta ya afya, ambapo kwa mwaka huu imekwisha tangaza ajira 10,280, ikiwajumuisha na wateknolojia dawa.
Katika hatua nyingine, Mtanda ametoa wito kwa viongozi wa kada hiyo kuwasilisha mapendekezo yao wizarani kuhusu namna bora ya kuongeza ajira na kubainisha maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wataalamu hao, kama ilivyoainishwa katika risala ya chama.



