Ziara ya Chongolo yaacha neema Mufindi Kusini
Vijiji 2 kupatiwa umeme, achangisha fedha za msikiti

MGENI njoo, mwenyeji apone’ msemo huu unaweza kutumika na wananchi wa Kata ya Malangali wilayani Mufindi mkoani Iringa baada ya ziara iliyofanywa na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo kuwezesha kupatikana kwa umeme Kwa vijiji vya Mjimwema na Ibangi.
Ziara ya Chongolo haijasaidia upatikanaji kwa umeme tu bali kuwezesha ujenzi wa msikiti wa Malangali kukamilika
Akitoa maagizo ya ukamilishaji ya masuala hayo leo Mei 29,2023 katika Kata ya Malangali, Chongolo aliagiza vijiji vya Mjimwema na Ibangi kupatiwa umeme mara moja kwa kuwa bajeti ipo.
Pia, alimuagiza Mbunge wa Mufindi Kusini ambae pia ni Mwenyekiti wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, David Kihenzile kutoa sh milioni 3, mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Leonard Mahenda ‘ Qwihaya’ kutoa sh milioni 2 na yeye mwenyewe amehaidi kutoa sh milioni 4 ili kumalizia ujenzi wa msikiti wa Malangali.
Kuhusu kilio cha wananchi ambao waliomba barabara ya kiwango cha changarawe kutoka Mbaramaziwa kwenda Ihohanza, Chongolo aliagiza Tanroad kufanya tathmin ili iweze kutengewa bajeti.
Aidha, Chongolo ameshusha neema ya upatikanaji maji safi na salama katika vijiji tisa vya Malangali, Ihohanza na Idunda ambapo mkataba wa kuanza mradi huo utasainiwa rasmi Juni 15.
Pia, alipokea hoja ya Mbunge wa Jimbo la Mafundi Kusini, David Kihenzile ya ujenzi wa kituo cha afya na gari maalum ya kubeba wagonjwa (Ambulance).
“Nimpongeze Mbunge wa Jimbo hili Mh Kihenzile amekua mstari wa mbele kupigania maendeleo ya wananchi wa Jimbo hili, pili naiagiza halmashauri kujenga kituo cha afya haraka ili nipush serikali ilete vifaa ikiwemo x-ray . ” Amesema