Dk. Mwinyi aongoza dua maalumu ya amani

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amejumuika na walimu wa madrasa, masheikh na uongozi wa Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar katika dua maalumu ya kumuombea yeye, taifa pamoja na Uchaguzi Mkuu ujao.

Dua hiyo imefanyika katika Ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein, Tunguu, Mkoa wa Kusini Unguja, ikiandaliwa na Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar kwa kushirikiana na Jumuiya ya Kuendeleza Walimu wa Vyuo vya Qur’an Zanzibar (JUKUWAVOQUZA).

Akizungumza katika hafla hiyo, Dk. Mwinyi amewataka wananchi kuendelea kuiombea nchi amani, akibainisha kuwa hali hiyo ndiyo nguzo kuu ya maendeleo na ustawi wa taifa. Amesema kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 kinahitaji umoja na utulivu, hivyo kila mmoja ana wajibu wa kudumisha amani.

Aidha, amewakumbusha viongozi wa dini, wanasiasa na wanahabari, ambao ni miongoni mwa makundi yenye ushawishi mkubwa katika jamii, kuhakikisha wanatumia nafasi zao kuhubiri amani na mshikamano. SOMA: Tuache chokochoko tudumishe amani

Rais Mwinyi amepongeza kuanzishwa kwa Jumuiya ya Walimu wa Madrasa, akisema ni hatua muhimu ya kuwaunganisha walimu wa Qur’an chini ya chombo kimoja kwa lengo la kuimarisha malezi na maadili ya Kiislamu kwa watoto na vijana. Amesema jumuiya hiyo ni nguzo ya maadili mema inayowasaidia vijana kujengeka katika misingi ya uadilifu, uzalendo na uchapa kazi kwa manufaa ya taifa.

Vilevile, Dk. Mwinyi ameshauri kuandaliwa kwa mitaala maalumu ya kufundishia elimu ya dini ili kuhakikisha kunakuwepo na mwongozo unaofanana katika taasisi zote za dini nchini. Katika hotuba yake, amesisitiza umuhimu wa kuangalia maslahi ya walimu wa madrasa kutokana na mchango wao mkubwa katika malezi ya watoto na jamii kwa ujumla.

Rais Mwinyi ameahidi kwamba katika awamu ijayo ya uongozi wake, serikali itahakikisha walimu hao wanathaminiwa ipasavyo kwa kazi yao ya kujitolea katika kujenga jamii yenye maadili bora.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button