NAIBU Waziri wa Afya, Dk Godwin Mollel amesema serikali itachukua hatua kali kwa wote wataobainika kwenye upotevu wa dawa ili kutoa funzo kwa wengine.
Akizungumza jijini Dodoma leo Mei 23, 2023 Dk Mollel amesema wanaofanya mambo hayo wanawakosesha wananchi haki yao ya msingi ya huduma kwenye vituo vya kutolea huduma na hivyo hawatawafumbia macho.
Akifafanua amesema wizara hiyo iliona dalili za upotevu wa Sh bilioni 83 na hivyo kushirikiana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ili kuhakikisha wote wataobainika kuwepo katika upotevu huo wa dawa wanachukuliwa hatua.
“Serikali imefanya mikakati mbalimbali katika kutatua tatizo la wizi na ubadhilifu wa dawa na vifaa tiba ikiwemo kufanya suala la upotevu wa dawa na vifaa tiba kama agenda katika vikao vya Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa na Wilaya,” alisema Dk Mollel.
Aidha, naibu waziri huyo amesema serikali imeendelea kuimarisha mifumo ya usimamizi wa bidhaa za afya ikiwemo kufunga mifumo ya kieletroniki pamoja na kufanya ufuatiliaji wa mara kwa mara wa bidhaa hizo.