Waandishi kupigwa msasa habari za uchunguzi

ARUSHA; SHIRIKA la Utangazaji la kimataifa la Aljazeera limekubali kushirikiana na Chama Cha Wafanyakazi katika Vyombo vya habari nchin i(JOWUTA) kutoa mafunzo kwa wanahabari ya usalama kazini na uandishi wa habari za uchunguzi.
Makubaliano hayo yamefikiwa katika wa mkutano wa wanahabari Afrika , ulioandaliwa na Shirikisho la Kimataifa la Waandishi wa habari Afrika (IFJ), ikiwa ni mfululizo wa vikao vinavyoendana na kikao cha 77 Cha Tume ya Afrika ya Haki za Binaadamu na Watu(ACHPR) ambavyo vinaendelea jijini Arusha.
Mkurugenzi wa Aljazeera wa masuala ya Jamii na Haki za Binaadamu,Sami Elhag amesema Aljazeera ipo tayari kusaidia wanahabari Tanzania ili kufanya kazi kwa ufanisi.
Elhag amesema miongoni mwa maeneo ambayo wataweza kusaidia ni mafunzo kwa wanahabari katika masuala ya usalama, jinsi ya kuandika habari za uchunguzi, kuboresha Utendaji wa kazi na kubadilishana uzoefu..
Amesema wanahabari duniani wanakabiliwa na changamoto nyingi za kiusalama na tayari kituo cha Aljazeera, wanahabari wake wamepatwa na changamoto mbalimbali.
Ahadi hiyo ya Aljazeera ilitolewa kutokana na maombi ya Mwenyekiti wa JOWUTA, Mussa Juma kuomba wanahabari nchini kupata fursa ya mafunzo na ziara za kubadilishana uzoefu.

Juma amesema, wanahabari wanakabiliwa na changamoto za kiusalama wakiwa kazini hasa wanapokwenda kuandika habari sehemu zenye migogoro, maslahi duni, wengi hawana ujuzi wa kutosha wa uandishi wa habari za uchunguzi na Vita na kukabiliana na majanga.
Awali Katibu wa IFJ, Louis Thomasi amesema wanahabari maeneo mengi duniani wanakabiliwa na changamoto za kiusalama kazini, lakini pia na uwepo wa sheria ambazo ni kandamizi.
Amesema kuna haja ya wanahabari kupatiwa mafunzo ya kiusalama, lakini kupatiwa huduma muhimu ikiwepo maslahi na kuwepo sheria ambazo zitakuza Uhuru wa Vyombo vya habari na Uhuru wa kujieleza.
Thomasi alitaka Serikali barani Afrika kuwa na sheria rafiki ambazo zinasaidia wanahabari kufanya kazi vizuri na hivyo kuchangia ukuaji wa demokrasia na Maendeleo.
Awali Mwakilishi wa Shirika la kimataifa la A19, Alfred Bulakali amesema hakuna demokrasia kwenye taifa lolote bila kuwepo uhuru wa vyombo vya habari na uhuru wa kujieleza.



