Watafiti wa Tanzania kupata fursa mpya kimataifa

TUME ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) imeshiriki katika Mkutano wa Programu ya u’GOOD, inayofadhiliwa na Baraza la Utafiti la Afrika Kusini (National Research Foundation), Human Sciences Research Council, pamoja na Botnar Foundation kutoka Uswisi.

Programu hiyo inalenga kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika sekta ya utafiti, ambapo Tanzania ni miongoni mwa nchi 12 zinazoshiriki katika utekelezaji wa miradi ya kisayansi na kijamii kupitia programu hiyo. Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Utafiti wa COSTECH, Dk. Bugwesa Katale, amesema kuwa katika programu hiyo jumla ya maandiko ya miradi 120 yaliwasilishwa kutoka nchi mbalimbali, ambapo miradi 23 ilichaguliwa kupata ufadhili.

Alibainisha kuwa Tanzania imefanikiwa kupata miradi nane ambayo watafiti wa ndani watatekeleza kwa kushirikiana na wenzao kutoka nchi nyingine tisa zilizoshinda. “Sisi kama nchi tumefanikiwa kupata jumla ya miradi nane ambayo watafiti wetu watatekeleza kwa kushirikiana na watafiti kutoka nchi nyingine tisa zilizofanikiwa kushinda,” alisema Dk. Katale.

Kwa mujibu wa Dk. Katale, ushiriki wa Tanzania katika programu hiyo ni hatua muhimu kwa maendeleo ya sekta ya utafiti na ubunifu nchini. Amesema programu ya u’GOOD inawaunganisha watafiti wa Tanzania na wenzao kutoka nchi mbalimbali kusini mwa Jangwa la Sahara na Asia, jambo litakalosaidia kubadilishana uzoefu, kukuza ujuzi na kuimarisha uwezo wa kitaalamu katika nyanja za kijamii, kiteknolojia na kisayansi.

“Hii ni fursa ya kipekee kwa watafiti wetu kushirikiana kimataifa, kubadilishana uzoefu na kukuza ujuzi katika maeneo mbalimbali ya kijamii, kiteknolojia na kisayansi,” aliongeza.

Dk. Katale ameendelea kusisitiza kuwa programu hiyo ni chachu ya maendeleo ya kitaaluma na kijamii nchini, kwani inatoa mwamko mpya wa ushirikiano wa kimataifa unaolenga kutumia matokeo ya utafiti katika kuboresha maisha ya wananchi. “Kupitia ushirikiano huu, watafiti wetu watapata nafasi ya kushiriki katika tafiti zenye athari chanya kwa jamii na kuchangia katika ajenda za maendeleo endelevu,” alisema.

Kwa ujumla, ushiriki wa COSTECH katika programu ya u’GOOD unaonesha dhamira ya Tanzania kuendelea kuwekeza katika utafiti na maendeleo ya sayansi. Kupitia mpango huu, nchi itaweza kuimarisha uwezo wa watafiti wake, kuongeza ubunifu, na kuleta suluhu endelevu katika masuala ya kijamii na kiuchumi.

Hatua hii pia inaendana na dira ya taifa ya kujenga jamii inayotumia sayansi na teknolojia kama nyenzo kuu ya maendeleo. SOMA: RC: Sayansi na Teknolojia kichocheo mapinduzi ya kilimo, viwanda, afya

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button